Taarifa zinasema ndege hiyo imetunguliwa katika Miinuko ya Golan wakati kikosi cha ulinzi wa anga cha Jeshi la Syria kilipovurumisha makombora kukabiliana na uvamizi wa Israel dhidi ya kituo cha ndege za kijeshi kati mwa Syria. Afisa hiyo aidha amedokeza kuwa, ni zaidi ya ndege moja ilivyotunguliwa.
Jeshi la utawala haramu wa Israel limethibitisha kuwa, ndege yake ya kivita aina ya F-16 imedondoshwa kaskazini mwa ardhi zinazokaliwa kwa mabavu na Israel na kuongeza kuwa, marubani waliweza kuruka kwa mwavuli kutoka ndani ya ndege hiyo kabla haijaanguka na kuteketea kikamilifu. Taarifa zinasema hali ya rubani huyo wa Kizayuni ni mahututi.
Wakati huo huo Fawzi Barhoum Msemaji wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina, Hamas, amepongeza hatua ya Syria kutungua ndege hiyo ya Israel na kusema ni jibu tarajiwa kwa hujuma ya utawala huo.
Harakati ya Hizbullah ya Lebanon nayo imesema kutunguliwa ndege hiyo ya kisasa ya Israel ni jambo linaloashiria kuingia duru mpya ya kistratijia ambapo itakuwa vigumu kwa ndege za kizita za Israel kukiuka anga ya Syria. Hezbollah imelaani uvamizi wa Israel katika ardhi ya Syria sambamba na kutangaza kusimama pamoja na watu wa Syria katika mapambano yao.