IQNA

Wairani zaidi ya milioni 3 kushiriki matembezi ya Arubaini ya Imam Hussein AS

9:24 - October 12, 2019
Habari ID: 3472168
TEHRAN (IQNA) – Wairani zaidi ya milioni tatu wamejisajili kushiriki katika matembezi ya Arubaini ya Imam Hussein AS mwaka huu.

Kwa mujibu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Iran, Wairani milioni 3.83 hadi sasa wameshajisajili katika tovuti maalumu inayojulikana kama Samah kwa ajili ya kushiriki katika  Ziyara na Matembezi ya Arubaini ya Imam Hussein AS nchini Iraq.

Taarifa hiyo imesema mkoa wa Tehran una watu 489,000 waliojisajili, hii ikiwa ni idadi kubwa zaidi hadi sasa ikifuatiwa na mikoa ya Khuzestan, Isfahan, Khorassan Razavi na Fars. Siku ya mwisho ya kujisajili ni Alhamisi Oktoba 17.  Tayari Wairani zaidi ya milioni mbili wameshaingia Iraq kwa ajili ya kushiriki katika matembezi ya Arubaini ya Imam Hussein AS ambaye yametajwa kuwa kati ya mijumuiko mikubwa zaidi ya kidini duniani ambapo mwaka jana inakadiriwa kuwa watu milioni 20 walishiriki na idadi hiyo inatazamiwa kuongezeka mwaka huu.

Inafaa kuashiria hapa kuwa, tarehe 20 Safar inasadifiana na kutimia Arubaini ya kuuawa shahidi Mjukuu wa Mtume Muhammad SAW,  Imam Hussein AS pamoja na wafuasi wake 72. Imam Husain AS aliuawa shahidi kikatili na kinyama tarehe 10 Muharram mwaka wa 61 Hijria, yaani miaka 1380 iliyopita, katika jangwa la Karbala, Iraq ya leo, akiwa na umri wa miaka 57 baada ya kuongoza mapambano ya kishujaa ya ushindi wa damu mbele ya upanga.

Vita vya Karbala vilikuwa moja kati ya vita mashuhuri katika historia ya Kiislamu na ya mwanadamu, vilitokea baina ya majeshi ya haki na batili katika ardhi ya Karbala huko Iraq. Siku aliyouawa shahidi Imam Hussein AS inajulikana kwa jina la Ashura.

3848999

captcha