IQNA

Apple yashinikizwa na China kuondoa apu maarufu ya Qur'ani Tukufu

11:48 - October 17, 2021
Habari ID: 3474435
TEHRAN (IQNA)- Shirika la Kimarekani la Apple ya limeondoa aplikesheni ya Quran Majeed katika simu zake zinazouzwa nchini China jambo ambalo limeibua maswali mengi juu ya malengo na sababu kitendo hicho.

Shirika la Apple limechukua uamuzi wa kushangaza wa kufuta apu hiyo yenye Qur'ani Tukufu kwa lugha asili ya Kiarabu na pia tarjuma kwa lugha nyinginezo pamoja na mafundisho mengine ya Kiislamu. Apu hiyo imefutwa kwenye jukwaa la App Store lenye kubeba aplikesheni zote za simu za iPhone na iPad. 

Kampuni ya Apple imedai kuwa imechukua hatua ya kuondoa apu ya Quran Majeed katika bidhaa zake nchini China ili kutiii amri ya serikali ya Beijing. Hata hivyo serikali ya China haijatoa maelezo yoyote kuhusiana na madai hayo.

Apu mashuhuri ya Quran Majeed hutumiwa sana kwa ajili ya qiraa ya Qur'ani na masuala mengine yanayohusiana na Swala kama kujua upande wa kibla, nyakati za Swala, dua, maeneo ya misikiti iliyo karibu na mtumiaji na kadhalika.

Shirika la Apple limetaka Shirika la Pakistan Data Management Services ambalo ndio mtegenezaji wa apu ya Quran Majeed kuwasiliana na wasimamzii wa intaneti China ili kusuluhisha tatizo hilo.

Katika miaka ya karibuni China imekuwa ikikabiliwa na ukosoaji mkubwa kuhusiana na ukiukaji wa haki za Waislamu hususan jamii ya Uighur katika jimbo la Xinjiang. Hatahivyo serikali ya China imekanusha kuwalenga Waislamu na inasema inakabiliana na watu wenye misimamo mikali ya kidini.

3476055

captcha