IQNA

Fikra za Kiislamu

Tahaddi: Qur’ani Tukufu inawaita wakanushaji kwenye changamoto

23:09 - September 09, 2022
Habari ID: 3475758
TEHRAN (IQNA) – Qur’ani Tukufu ni muujiza wa milele na iko katika kiwango cha juu cha ufasaha na maudhui. Njia moja ambayo Qur’ani Tukufu inaitumia kuimarisha nyoyo za waumini ni Tahaddi (kukaribisha changamoto).

Neno Tahadi lina maana ya kumpa mtu changamoto na pia linarejelea tukio la kihistoria wakati Mtukufu Mtume Muhammad  (SAW) aliposoma Qur’ani Tukufu, Mushrikin (washirkina) hawakumwamini na walifikiri kuwa si neno la Mwenyezi Mungu bali ni hadithi zilizotungwa na Mtukufu Mtume (SAW).

Kwa hiyo, Mwenyezi Mungu akawapa changamoto Mushrikin kuleta kitabu kama Qur’ani: “ Sema: Wangeli kusanyika watu na majini ili walete mfano wa hii Qur'ani basi hawaleti mfano wake, hata wakisaidiana wao kwa wao..” (Surah Al-Isra, Aya ya 88).

Hata hivyo hakuna mtu aliyekuwa na uwezo wa kufanya hivyo na, kwa hiyo, Mwenyezi Mungu akaifanya rahisi zaidi, akiwaita Mushrikin kuleta Sura kumi, kisha Sura moja tu kama zile za Qur’ani. Bado, hawakuweza kuifanya.

“Je! Ndiyo wanasema ameizua? Sema: Hebu leteni sura moja mfano wake na muwaite (kukusaidieni) muwawezao, isipo kuwa Mwenyezi Mungu, ikiwa nyinyi mnasema kweli.” (Sura Yunus, Aya ya 38).

Katika historia ya Uislamu, Tahadi ni uthibitisho wa ukweli wa Mtukufu Mtume (SAW) na huonyesha kuwa Qur’ani haikuwa kitabu kilichoandikwa na mwanadamu bali kimetoka kwa Mwenyezi Mungu na hakuna kitu mfano wake katika ardhi.

Vile vile ilizichangamsha nyoyo za wale ambao walikuwa na mashaka fulani juu ya ujumbe wa Mtukufu Mtume (SAW), kuwafanya wawe na uhakika kwamba ametumwa na Mwenyezi Mungu na yale aliyoyasema yametoka kwa Mwenyezi Mungu.

Zaidi ya hayo, Tahaddi ilifungua njia ya uenezaji wa dini na ukuzaji wa ujumbe wa Qur'ani Tukufu kwa sababu Mushrikin walishindwa kuthibitisha madai yao kwamba maudhui ya Qur'an yalitokana na ngano za kale.

Tahaddi ilikuwa ni mwaliko wa changamoto iliyowafanya Mushrikin kunyamaza mbele ya ukweli na ikathibitisha Qur’ani Tukufu kuwa njia ya furaha, saada na wokovu katika ulimwengu huu na kesho akhera.

captcha