IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu

Uadui wa Marekani na Iran unaendelea

20:32 - March 20, 2016
Habari ID: 3470207
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza kuhusu kuendelea uadui wa Marekani na taifa la Iran na kusema kuwa, 'Jamhuri ya Kiislamu ya Iran haitalegeza msimamo kuhusu misimamo yake ya kimsingi.'

Ayatullah Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameyasema hayo alipohutubua makumi ya maelfu ya watu na wafanyaziara katika Haram Takatifu ya Hadhrat Ali bin Musa Ridha AS, Imam wa nane wa Waislamu wa madhehebu ya Shia katika mji mtakatifu wa Mashhad kaskazini mashariki mwa Iran. Kiongozi Muadhamu ameongeza kuwa, Marekani inataka Jamhuri ya Kiislamu ya Iran isitishe uungaji mkono wake kwa waliodhulumiwa katika eneo, taifa la Palestina, Ghaza, Yemen na Bahrain. Amesisistiza kuwa, wao (mfumo wa kibeberu ukiongozwa na Marekani) wameshindwa katika kadhia za Syria, Iraq na Palestina na wanaona kushindwa kwao huko kumesababishwa na Iran. Ayatullah Khamenei ameashiria ukuruba na kushirikiana baadhi ya nchi na serikali za eneo na utawala wa Kizayuni wa Israel na kusema wanataka Jamhuri ya Kiislamu ya Iran nayo iwe pamoja na utawala huo. Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema matakwa ya Marekani kwa Iran yana maana kuwa, Jamhuri ya Kiislamu iende sambamba na matakwa ya Marekani na hata iachane na uwezo wake wa kujihami.

Ayatullah Khamenei ameashiria namna Marekani inavyoikosoa Iran kutokana na kufanyia majaribio makombora yake pamoja na mazoezi ya kijeshi na kusema, Marekani hufanya mazoezi ya kijeshi mara kwa mara katika Ghuba ya Uajemi kwa kushirikiana na mojawapo ya nchi za eneo katika hali ambayo eneo hili liko mbali sana na Marekani na pia pamoja na kuwa Washington haina jukumu lolote katika eneo.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu pia ameashiria mapatano ya nyuklia yajulikanayo kama Mpango Kamili wa Pamoja wa Utekelezaji (JCPOA) baina ya Iran na madola sita yenye nguvu zaidi duniani na kusema, Marekani haijatekeleza ahadi zake katika mapatano hayo ya nyuklia na ingali inaendeleza vikwazo dhidi ya Iran. Ameongeza kuwa, harakati ya kimapinduzi na uchumi wa kimuqawama (kimapambano) ni nukta ambazo zitaiokoa Iran na kusisitiza kuwa, iwapo nukta hizo zitatekelezwa basi vikwazo vya Marekani dhidi ya Iran havitakuwa na taathira.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameashiria njia mbili za kuchagua kwa mtazamo wa mfumo wa kibeberu ambazo ni ima kusikilizana na Marekani au kustahamili daima mashinikizo ya Marekani na matatizo yatokanayo na mashinikizo hayo na kusema: "Kwa Uchumi wa Muqawama (mapambano); Hatua na Utekelezaji tunaweza kusonga mbele." Ayatullah Khamenei amesistiza kuwa, vijana wa Iran wanapaswa kufahamu kuwa iwapo watajitokeza katika medani na wakajiamini, Marekani na hata mkubwa zaidi ya Marekani hatoweza kufanya ghalati yoyote.

3484209

captcha