IQNA

Polisi ya Afrika Kusini yaomba msamaha baada ya afisa wake kuuvunjia heshima Uislamu

12:37 - April 27, 2020
Habari ID: 3472709
TEHRAN (IQNA) – Waziri wa Polisi Afrika Kusini Bheki Cele amewaomba radhi Waislamu nchini humo baada ya afisa wa polisi kutamka matamshi ya kuvunjia heshima Uislamu wakati akiwakamata waumini waliokuwa wamekiuka sheria za kuzuia mijimuiko kutokana na janga la corona.

Cele ameomba radhi baada ya klipu vya video kuenea katika intaneti ikionyesha namna polisi walivyowakamata waumini 24 katika mkoa wa Mumalanga Jumamosi.

Mwishini mwa klipu hiyo, afisa wa polisi alisikika akiwauliza waumini: "Nyingi ni wakubwa kumliko rais?, Je Mtume Muhammad ni mkubwa kumliko rais?

Hivi sasa kote Afrika Kusini kunatekelezwa sheria ya kutotoka nje na kuzuia mjumuiko ambayo ilitangazwa na Rais Cyril Ramaphosa mnamo Machi 27 ili kuzuia kuenea ugonjwa wa corona.

Kwa mujibu wa sheria hiyo watu hawaruhusiwa kutoka majumbani mwao au kujumuika katika makanisa na misikiti.

Msemaji wa Kitaifa wa Polisi Afrika Kusini Vishnu Naidoo amesema matamshi ya afisa huyo wa polisi ni ya kusikitisha na hayakubaliki. Amesema Idara ya Polisi imeamuru tukio hilo lichunguzwe na mhusika au wahusika waadhibiwe.

Hadi kufikia Aprili 27 Afrika Kusini ilikuwa na kesi 4,546 za maamubukizi ya corona ambapo watu 87 wamefariki na wengine 1, 473 wamepata afueni.

3894544

captcha